Monday, April 16, 2012

MAADILI YA UVAAJI WA MAVAZI KWA VIJANA


WANAFUNZI ELIMU YA JUU WATAMBUE MAVAZI NI SEHEMU YA MAADILI
HIVI karibuni kulitolewa  taarifa za kupiga marufuku uvaaji wa mavazi ambayo ni kinyume cha maadili kwa vijana wa kitanzania.Ni baada ya uongozi wa Chuo cha Biashara (CBE) kuwatolea uvivu baadhi ya wanafunzi katika  kampasi zake  kwa kutoa onyo kali na kutowaruhusu kuingia katika eneo la kitaaluma. Ni matumaini yangu kwamba taarifa iliwafikia ipasavyo walengwa  kuhusu maadili ya namna ya uvaaji kwa wanafunzi wa vyuo.

Hii ilitokana na kukithiri kwa uvaaji holela wa mavazi yasiyo rasmi, hivyo baadhi ya wahadhiri wa chuo hicho kulalamikia suala hilo. Baada ya uongozi wa chuo kubaini kumekuwapo na ukiukwaji wa maadili, kutumia vibaya uhuru wa uvaaji mavazi waliopewa na kupelekea wakati mwingine kuingia darasani na mavazi yasiyo rasmi.  Uongozi wa chuo hicho ndipo  ukaamua wanafunzi kuvaa mavazi  rasmi na kwamba ambaye hatakuwa tayari kufuata utaratibu huo uliowekwa atasimamishwa masomo kwa takriban miezi mitatu na mwanafunzi atakayefika maeneo ya chuo akiwa hajavaa mavazi hayo rasmi hatoruhusiwa kuingia katika eneo la chuo.

Hii ni taarifa nzuri kwa vijana hasa wale ambao wanatarajia kujiunga na vyuo vikuu na wale walio katika elimu za chini kama msingi na sekondari. Iwapo uamuzi huu utatekelezwa vizuri ni dhahiri kwamba wanafunzi watakaojiunga na vyuo nao wataukuta utaratibu huo na watauendeleza. Hii itawawezesha kuzoea uvaaji huo wa mavazi rasmi na kuwa utamaduni wa wanafunzi wa vyuo na taasisi nyingine za elimu.

Mara nyingi nimekuwa najiuliza kwa nini  vijana wengi wapo nje ya maadili. Je, ni kukosa elimu stahili juu ya maadili au ni kujifunza maadili ya watu wa Magharibi kwani ni kweli kwamba mambo wanayoyafanya vijana kwa sasa ni maeneo mengi yameathiriwa na uigaji kutoka tamaduni za mataifa yaliyoendelea.

Labda tufunguane macho na fikra juu ya suala hili la maadili, kwa kuiangalia tu maana ya maadili wewe kama kijana uaweza ukajua ni wapi unakosea na wapi haukujifunza tangu ukiwa mtoto hadi kufikia umri ulionao hivi sasa.  Jifunze sasa…Ni dhahiri kwamba, Maadili ni mafundisho na mwongozo yanayopatikana sehemu mbalimbali na katika nafasi mbalimbali kama vile katika malezi,  lengo likiwa ni kutaka kumuelekeza binadamu atende kwa namna ambayo itamjenga yeye pamoja na jamii nzima inayomzunguka na kwamba maadili katika jamii ni yale yale  ila yanaweza kutekelezwa kwa namna tofauti kutokana na mazingira tofauti. Je wewe kijana ulikuwa unajua hilo?

Labda turudi nyuma enzi za mababu zetu ambako ni dhahiri kwamba kuna utofauti kati ya ‘ukale na usasa’. Hapo awali enzi za mababu zetu tunaona kuwa maadili yalikuwamo na yalikuwa yanatolewa kwa namna maalumu kulingana na imani ya dini, utamaduni wa sehemu fulani au hata falsafa na taratibu za kimaisha za jamii fulani. Kumfundisha mtoto maadili ilikuwa ni jambo muhimu kwani ilimuandaa kuwa imara wakati atakapofikia umri wa yeye mwenyewe kujitegemea katika maisha. Pia ilimsaidia katika kujua mabaya na mazuri yanayomzunguka ikiwa ni pamoja na adabu na hekima ndani ya jamii yake.

Chanzo cha kupotea kwa maadili kwa mtazamo wangu naona ni kutokana na huu utandawazi ambapo ni wazi sayansi na teknolojia zimekuwa kwa kasi na hivyo kuwaathiri watumiaji ambao kwa kiasi kikubwa ni vijana. Ni dhahiri kwamba uwepo wa teknolojia hizi ambazo ni pamoja na runinga, kompyuta, simu na nyinginezo, ndizo zilizosababisha kupoteza kabisa maadili ya vijana wa Kiafrika.
Katika suala la uvaaji sidhani kama kuvaa milegezo na kusuka nywele kwa wanaume ni asili ya Mwafrika, pia uvaaji wa nusu uchi na kupita mbele za watu tena bila ya kuwa hata na chembe ya uoga ni utamaduni wa Mwafrika.
Huku ni kuiga tu kwa wenzetu wa Mataifa ya Magharibi hasa Ulaya na Marekani. Tujivunie uafrika wetu na kuvaa mavazi yetu ya asili na kuacha kuwaiga. Hivi hatujiulizi kwamba wao hawaigi mavazi yetu?  Kama hujui basi achana na mazoea ya kuiga mavazi yao na tuvae mavazi ya kwetu kwani kwa kipindi hiki wao ndiyo wanaoiga uvaaji wa mavazi ya kiafrika na kuachana na mavazi yao. Huoni kama ni jambo la kujivunia kwa Waafrika? Chunguza baadhi ya Wasanii, watu maarufu wa Marekani na Ulaya na watalii wanaofika katika nchi yetu utapata jibu.
Baadhi ya mavazi hayo ni mavazi ya kitenge, batiki na khanga na wanatamani sana yawe ndiyo mavazi yao ya asili.
Mi naona tunataka tuipuuze asili yetu ya tulikotoka, kama wao wana asili yao kwa nini na sisi tusiitukuze asili yetu Waafrika?
Elimu tunayoipata darasani tukichanganya na maadili kutoka kwa waliotutangulia na tukiyazingatia ni wazi tutafika kule tuendapo na kuwa kama kioo cha wadogo zetu wanaotufuata. Tukianza sisi leo kama tulivyoyakuta kwa waliotutangulia ni wazi kwamba hata wadogo zetu watayaendeleza na kurudisha ustaarabu wa Kiafrika unaosifika kwa maadili mazuri.
Kama Serikali inavyofanya mchakato wa kutafuta Vazi la Taifa, inapasa hata katika Taasisi za Elimu kutumia mavazi hayo ili kuwatambulisha na kuwatofautisha wanafunzi wa watu wengine na hii itasaidia  katika kuujenga upya utamaduni wa Mtanzania ambao umekuwa ukipotea siku hadi siku kutokana na uingiaji wa sayansi na teknolojia.
Tunaweza tukiamua,vijana tuamke na tuzingatie maadili yaliyo bora,tujiheshimu katika uvaaji, kwani kuiga ni ushamba tofauti na jinsi wengi wanavyodhani kwamba kuvaa mavazi ya asili ni ushamba na kuiga ni kwenda na wakati.

GET UP YOUTH 

1 comment:

  1. Tusisahau tulikotoka kwa kuiga ya mbele...tutapotea....GET UP.

    ReplyDelete